Mwanamke aliyetambulika kwa jina la Silvia Chapa (30), mkazi wa Meresini mjini mdogo wa Himo wilayani hapa,mkoani Kilimanjaro ameuawa na mtu anayeaminika kuwa mumewe kwa kuchinjwa mithili ya kuku hadi kufa na kisha mumewe kunywa sumu kwa lengo la kujiua.


Kamanda wa Polisi mkoani hapa Robart Boaz amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema, limetokea usiku wa kuamkia Novemba 22,mwaka huu ambapo mwili wa mwanamke huyo uligundulika majira ya mchana ukiwa umefungiwa ndani ya nyumba.
Kamanda amemtaja mwanaume aliyefanya mauaji hayo kuwa ni Michael Alfonce (28) ambaye baada ya kufanya mauaji hayo alikunywa sumu inayoaminika kuwa ni ya panya, kisha kufunga mlango na yeye kutoka nje ya nyumba na kulala chini.
Majirani ndiyo waliomwona Alfonce akiwa amelala chini wakampigia simu tajiri yake ambaye alifika na kumkimbiza hospitali lakini akamuuliza alikoweka ufunguo wa nyumba alipomuagizia alirudi nyumbani na kufungua mlango na kukutana na mwili wa mwanamke huyo,”alisema Kamanda.
Kamanda huyo alisema, mwanaume huyo anauza duka la Godfrey Machange ambaye alifungua nyumba yake na kukuta damu imetapakaa ndani ya nyumba huku mwili wa mwanamke huyo ukiwa chini. Mwanaume huyo inadaiwa alifanya mauaji hayo akiwa na lengo la yeye kujiua pia lakini hakufanikiwa kwa kuwa amewahiwa na kukimbizwa hospitalini ambako amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC mjini Moshi na kwamba hadi sasa chanzo cha mauaji hayo hakijafahamika.
Mmoja wa majirani aliyetambulika kwa jina moja la Massawe alisema, wawili hao walikua na ugomvi wiki iliyopita lakini alirudi siku ya Jumanne baada ya kikao cha usuluhishi na kwamba wanashangaa kuona baada ya siku moja mwanaume huyo ameamua kumchinja mkewe mithili ya kuku na yeye kutaka kujiua.

Alisema katika familia hiyo wamebarikiwa kuwa na mtoto mmoja ambaye bado ni mdogo na kwamba wakati wa mauji hayo mtoto huyo hakuwapo kwa kuwa walimwacha kwa bibi yake.


Post a Comment

POPULAR POST

 
Top